Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga amefanya mazungumzo na Mawaziri wawili wa Serikali ya Uturuki ambao ni Waziri wa Viwanda na Teknolojia, Mhe. Mehmet Fatih Kacır; na Waziri wa Biashara, Prof. Dkt. Ömer Bolat. Mazungumzo hayo yalifanyika jijini Istanbul, Uturuki Juni 06, 2026.

Mazungumzo na Waziri wa Viwanda na Teknolojia yalijikita katika kuimarisha ushirikiano wa maendeleo ya viwanda vya kimkakati wenye lengo la kukuza mchango wa sekta hiyo na kuhamasisha matumizi ya teknolojia. Kupitia mazungumzo hayo, Tanzania ilitambua mchango wa sekta ya viwanda katika uchumi na ilieleza nia yake ya kushirikiana na Uturuki ili kufikia azma ya malengo ya Dira 2050 ya kipato cha kati cha juu. Akiunga mkono dhamira ya Tanzania, Waziri Kacir alimthibitishia Waziri Kapinga kuwa Serikali ya Uturuki itashirkiana na Serikali ya Tanzania katika kuibua fursa mbalimbali za kukuza sekta ya viwanda hasa kwa kuzingatia teknolojia rafiki kwa mazingira ambayo pamoja na mambo mengine inapunguza uzalishaji wa taka na kutumia nishati safi itokanayo na vyanzo rafiki kwa mazingira.


Aidha, Waziri Kapinga, alitumia fursa ya mazungumzo hayo kuelezea vipaumbele vya Tanzania katika kuleta mageuzi ya viwanda pamoja na kuhamasisha wawekezaji kutoka nchini humo kuja kuwekeza Tanzania katika sekta ya viwanda vya uzalishaji na vile vya kuongeza thamani malighafi za kilimo na madini. Miongoni mwa maeneo yaliyotiliwa mkazo ni viwanda vya chuma, dawa za binadamu na vifaa tiba, akili unde, chakula na kongani za viwanda vya kijani (green industrial parks).


Mawaziri hao walikubaliana kushirikiana katika kukuza ushirikiano wa kisekta kwa kubadilishana uzoefu, teknolojia na utaalamu ili kuleta tija katika uzalishaji. Vilevile, nchi hizi mbili zimekubaliana kushirikiana katika uendelezaji wa kongani za viwanda ili kuvutia uwekezaji, teknolojia na uzoefu kwa lengo la kuongeza mchango wa sekta ya viwanda katika maendeleo.